Zoezi la urejeshaji wa miundombinu ya barabara kuu ya Lindi - Dar es Salaam katika eneo la Somanga Mkoani Lindi ukiendelea ambapo timu ya wataalam kutoka Wakala wa Barabara (TANROADS) wanasimamia zoezi hilo kikamilifu ili kuruhusu mawasiliano kurejea kwa haraka.

Aprili 5,2024 Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa aliongea na wananchi waliokwama katika eneo hilo na kutoa taarifa yakuwa urejeshaji wa miundombinu ya barabara hiyo unatarajiwa kukamilika ndani ya saa 72 na kuweza kuruhusu magari na wananchi kupita katika eneo hilo.








Waziri wa Uchukuzi Profesa Makame Mbarawa akiwasilisha Bajeti ya Wizara ya Uchukuzi na kutaja  mafanikio ya Shirika la Uwakala  wa Meli Tanzania (TASAC).

Baadhi ya watendaji wa Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Uchukuzi ikiwemo TASAC  wakifatilia Bajeti ya Wizara hiyo.

Na Mwandishi Wetu ,Dodoma

WAZIRI wa Uchukuzi Prof. Makame M. Mbarawa (Mb.) amesema Serikali kupitia Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) imeendelea kutoa huduma za udhibiti wa huduma za bandari, usafiri majini na kutoa huduma ya biashara ya meli kwa bidhaa mahsusi  Tanzania Bara.

Akizungumza wakati wa kuwasilisha bungeni Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha kwa Mwaka wa Fedha 2024/25 Mhe. Mbarawa amesema TASAC imeendelea kusimamia watoa huduma za usafiri kwa njia ya maji kwa kufanya tathmini na kutoa leseni na vyeti vya usajili kwa watoa huduma waliokidhi vigezo.

“Serikali kupitia TASAC imeendelea kutoa leseni na vyeti vya usajili kwa watoa huduma waliokidhi vigezo. Hadi kufikia Machi, 2024 jumla ya watoa huduma 1,722 waliosajiliwa na kupewa leseni ikilinganishwa na jumla ya watoa huduma 1,498 katika kipindi kama hicho kwa mwaka 2022/23 sawa na ongezeko la asilimia 14.95” amesema Mhe. Mbarawa.

Aidha ameongeza kuwa, katika kipindi cha kuanzia Julai, 2023 hadi Machi, 2024, Serikali kupitia TASAC imeendelea kurasimisha bandari bubu za Tanzania Bara ikiwa na lengo la kuimarisha  ulinzi na usalama katika maeneo ya bandari ili kuboresha utoaji wa huduma.

Aliongeza kuwa, jumla ya bandari bubu 99 zilikaguliwa na kufanyiwa tathmini ya kina na Serikali kupitia TASAC kwa kushirikishana na Mamlaka mbalimbali za  Serikali ambapo bandari 45 zilirasimishwa . 

Lengo la hatua hii ni kuhakikisha kuwa Serikali inaimarisha ulinzi na usalama katika maeneo ya bandari ili kuboresha utoaji wa huduma.

Kuhusu shughuli za utafutaji na uokoaji, Serikali kupitia TASAC imeendelea kuratibu shughuli hizo kupitia Vituo vya Utafutaji na Uokoaji Majini vilivyopo Dar es Salaam na Mwanza (Maritime Rescue and Coordination Centre – MRCC).

“Ili kuboresha usalama wa usafiri katika Ziwa Victoria, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Uganda chini ya uratibu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kupitia Kamisheni ya Bonde la Ziwa Victoria zimeendelea kutekeleza Mradi wa Kikanda wa Kuboresha Mawasiliano na Uchukuzi Katika Ziwa Victoria wenye lengo la kuimarisha huduma za utafutaji na uokoaji katika Ziwa” amesema Mhe. Mbarawa.

Hadi kufikia Machi, 2024 ujenzi wa Kituo Kikuu cha Kikanda cha Uratibu wa Masuala ya Utafutaji na Uokoaji katika Ziwa Victoria (Regional Maritime Rescue Coordination Centre - RMRCC) umefikia asilimia 26. Aidha, ujenzi wa vituo vidogo vitatu (3) vya utafutaji na uokoaji unaendelea.

SERIKALI imesema imebuni miradi mbalimbali ya kimazingira inayosaidia jamii kuweza kuhimili athari za mabadiliko ya tabianchi katika maeneo mbalimbali nchini.


Pamoja na hatua hizo pia, imeendelea kuihimiza jamii kutumia nishati mbadala na majiko banifu ili kupungunguza kasi ya ukataji wa misitu ambayo husababisha uharibifu wa mazingira.


Hayo yamesemwa na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Patrobas Katambi wakati akijibu maswali bungeni kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Jafo bungeni jijini Dodoma leo tarehe 06, 2024.


Akijibu swali la Mbunge wa Mwera Mhe. Zahor Mohammed Haji aliyetaka kujua mpango wa Serikali kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi katika kuwakinga wananchi na madhara yanayoweza kutokea, Mhe. Katambi amesema Serikali inatekeleza miradi ya upandaji miti, usambazaji wa maji safi kwa matumizi ya majumbani na mifugo na ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji.


Ametaja ujenzi wa kuta katika maeneo ya fukwe za bahari yanayokabiliwa na mmomonyoko wa ardhi, ujenzi matuta na mabwawa kudhibiti mafuriko, kuwezesha jamii kubuni miradi mbadala ya kuongeza kipato na iliyo rafiki kwa mazingira pamoja na urejeshaji wa maeneo ya ardhi yaliyoharibika kuwa ni jitihada zingine za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.


Akiendelea kujibu swali hilo, Mhe. Katambi amesema Serikali imeandaa Mkakati wa Kitaifa wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi (2021), Mpango Kabambe wa Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (2022-2032) na Mchango wa Taifa katika Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi (2021) ambayo ina mchango katika kukabiliana na changamoto hiyo.


Ameongeza kuwa Serikali inashirikiana kikamilifu na jumuiya ya kimataifa katika kubuni mikakati na hatua madhubuti za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi katika ngazi zote ikiwemo kuridhia Mkataba wa Umoja wa Mataifa Kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi, Itifaki ya Kyoto na Makubaliano ya Paris.


Aidha, Naibu Waziri Katambi amesema Serikali inaendelea kuelimisha wananchi kuhusu madhara yanayotokana na mabadiliko ya tabianchi ili waweze kuchukua tahadhari na kujilinda na maafa yanayosababishwa na changamoto hizo, ambapo uelimishaji hufanyika kabla ya maafa kutokea.


Waziri wa Ardhi. Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Jerry Slaa (wa pili kulia) akikata utepe kuzindua rasmi mradi wa nyumba kwa bei  nafuu wa Sky Royal Jijini Dar es Salaam. Wengine kutoka kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Coral Property Holding Co.Ltd  Zhou Tao, Mkurugenzi wa Ardhi wizarani, Upendo Matotola na Mkurugenzi Mkuu wa Hainan International Ltd Li Jun.
James Prevost akizungumza wakati wa kuzindua rasmi mradi wa nyumba kwa bei  nafuu wa Sky Royal Jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi  Mtendaji wa Coral Property Holding Zhou Tao akizungumza wakati wa kuzindua rasmi mradi wa nyumba kwa bei  nafuu wa Sky Royal Jijini Dar es Salaam.

Na Mwandishi Wetu
KATIKA mpango unaolenga kuunga mkono juhudi serikali za kuhakikisha kunakuwepo na nyumba za makazi bei, kampuni ya ya RE/MAX na ile ya Coral Property zimezindua mradi wa nyumba mpya za bei nafuu wa Sky Royal, mtaa wa Morocco Jijini Dar es Salaam.

Hafla ya uzinduzi wa nyumba hito iliyohudhuriwa na viongozi na wadau mbalimbali katika sekta ya nyumba, ambapo pamoja na mambo mengine, uzinduzi huo ulionyesha dhamira ya dhati ya ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi unaolenga kuwapatia watu makazi ya bei nafuu na yenye ubora wa hali ya juu.

Akizindua mradi huo, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Jerry Slaa, ameyapongeza makampuni hayo mawili kwa mpango huo ambao amesema umekuja wakati mufaka haswa ikitiliwa maanani ongezeko la uhitaji wa nyumba za makazi Jijini Dar es Salaam.

"Ujenzi wa nyumba za bei nafuu ni muhimu sana hapa nchini; uamuzi wa kampuni hizi mbili wa kujenga nyumba bora ni mfano bora w akuigwa na taasisi nyingine hapa nchini ili kukabiliana na changamoto inayohusiana na mahitjai ya nyumba bora za makazi”, amesema.

Waziri Silaa aliendelea kusema kuwa, hatua zilizochukuliwa na makampuni hayo mawili zinaunga mkono juhudi za Serikali zinazolenga kuwepo kwa nyumba bora za makazi na za gharama nafuu kwa wananchi hapa nchini.

"Nichukue fursa hii kutoa wito kwa wananchi kuchangamkia fursa hii ya nyumba nzuri za makazi; ni matumaini yangu kuwa uwekezaji wa nyumba nzuri za makazi katika soko kutaiwezesha Serikali kufikia azma yake ya wananchi kuwa na nyumba nchini”, amesema.

Aidha Waziri Silaa ametoa wito kwa makampuni ya RE/MAX Coastal na Coral Property kujiongeza na kupanua panua wigo wa uwekezji wao kwa kuwekeza maeneo mengine hapa nchini ikiwemo Jijini Dodoma ambapo amesema idadi ya watu inakuwa ikongezeka kila siku na hivyo kusababisha ongezeko la mahitaji ya nyumba za makazi na zenye gharama nafuu.

Tukio hilo mbali na kuwa la uzinduzi, pia lilitoa fursa ya washiriki kuona fursa za uwekezaji mzuri na wa uhakika uliofanywa na makampuni hayo.

"Washiriki watapata fursa ya kujionea wenyewe uwekezaji unaohusu nyumba zenye chumba kimoja, viwili na hata vitatu, ambazo zinagharimu kati ya dola za Marekani 81,186, USD 147,427, na USD 191,838; zaidi ya hayo, wawekezaji hao watatoa punguzo la asilimia 8 ya bei ya kila nyumba kama ilivyoorodheshwa, ambapo punguzo hilo litahusu siku ya uzinduzi tu”, imesema taarifa ya pamoja iliyotolewa na uongozi ma makampuni hayo mawili.

Akiongea katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Coral property Holdings Li Jun, amesema, “Uwekezaji huu umelenga kuunga mkono juhudi za Serikali zinazolenga kuhakikisha kunakuwa na nyumba nzuri za makazi na zenye bei nafuu; kupitia miradi ya maendeleo kama vile Sky Royal, pia tunalenga si kuwekeza kwenye nyumba tu, bali pia kuhakikisha wananchi wanakuwa na maisha endelevu, yenye ufanisi na ambayo yatachangia ustawi wa familia kwa ajili ya Watanzania.”

Amesema kampuni yake pia imejikita katika kuhifadhi na kulinda mazingira nakwamba mpango huo ni endelevu. Aidha amesema mradi huo wa Sky Royal unahusu mpango kabambe wa kiteknolojia unaolenga uwekezji wa nyumba bora unaohakikisha mazingira rafiki na kwamba mradi huo umeidhinishwa kituo cha uwekezaji nchini TIC.

Naye, Mkurugenzi wa Kanda wa kampuni ya RE/MAX Pwani, James Prevost, amesema, “Ushirikiano wetu na kampuni ya Coral Property Holdings hususan katika mradi huu wa Sky Royal, umetuwezesha kuwapatia wananchi Jijini Dar es Salaam maisha bora kupitia nyumba nzuri za makazi na zenye unafuu; punguzo la bei siku hii ya uzinduzi pia ni wito kwa wateja kunufaika na uwekezji wa huu mzuri”.

Amesema mradi wa Sky Royal haulengi uwekezaji wa nyumba za makazi tu, bali pia ni kielelezo cha uwekezaji wa nyumba nzuri na za uhakika ambao unalenga kutoa makazi mazuri na endelevu kwa wananchi na kwa bei nafuu.

"Eneo la kimkakati la maendeleo na huduma kamili kwa jamii, inalenga kutengeneza mazingira bora kwa wataalamu wa aina malimbali wakiwemo vijana, kwa wanafamilia na wamiliki wa biashara aina mablimbali," amesema.

Kampuni ya RE/MAX Coastal inasifika kwa utaalamu wake katika maswala ya mauzo na masoko ya majengo, ikiwa na dhamira ya kuwapatia wateja kilicho bora na chenye thamani kulingana na soko lililoko nchini Tanzania.

Kampuni ya Coral Property Holdings imekuwa mstari wa mbele katika kuendeleza uwekezaji wa uhakika wa majengo aina mbalimbali ikiwemo nyumba bora za makazi huku ikizingatia ubunifu wa hali ya juu na endelevu sambamba na ubora wa hali ya juu katika kuhakikisha kunakuweko na suluhisho la uhakika katika sekta ya makazi nchini Tanzania.

Ushirikiano kati ya RE/MAX Coastal na Coral Property Holdings kwenye uzinduzi wa mradi wa Sky Royal ni juhudi za kihistoria zinazolenga kuimarisha mandhari ya jiji la Dar es Salaam.

Kwa kuanisha malengo yao sambamba na ile ajenda ya Taifa inayolenga kuhakikisha uwepp wa makazi bora, kampuni zote mbili zimedhamiria kuimarisha sekta ya ujenzi hususani ujenzi wa majengo aina mbalimbali kwa lengo la kustawisha maisha ya Watanzania wote kwa ujumla.


Na Karama Kenyunko Michuzi Tv
SHUGHULI za Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), zimeendelea kuimarika na kutoa huduma za utabiri wa kila siku, siku kumi na ule wa muda mrefu pamoja na tahadhari ya matukio ya hali mbaya ya hewa ili kuhakikisha usalama wa watu na mali zao.

Kufuatia uboreshaji unaoendelea kufanywa na Serikali, usahihi wa utabiri umefikia asilimia 86 ambao ni juu ya asilimia 70 ya kiwango cha usahihi kinachokubalika na Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO).

Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa, amebainisha hayo leo, Mei 6,2024 jijini Dodoma wakati akiwasilisha utekelezaji wa bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha unaoisha wa 2023/24.

Amesema, TMA ilifanyiwa ukaguzi wa kimataifa kuanzia January 22 - 27, 2024, na kuendelea kukidhi vigezo vya kumiliki cheti cha ubora (ISO 9001: 2015).

61.

"Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020 Ibara ya 59(j) na Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa miaka mitano (FYDP III 2021/22-2025/26), Serikali iliahidi kuendelea kuimarisha miundombinu na huduma za hali ya hewa ikiwemo ununuzi wa rada" amesema Mbarawa.

Akielezea mafanikio ya TMA Prof. Mbarawa amesema Serikali kupitia TMA imefanikiwa kuendelea kuimarisha miundombinu na huduma za hali ya hewa, ikiwemo kwa kukamilisha ununuzi na ufungaji wa rada za hali ya hewa katika mikoa ya Kigoma na Mbeya na kufikisha jumla ya rada tano huku utengenezaji wa rada nyingine mbili (2) unaendelea kiwandani nchini Marekani na zinatarajiwa kukamilika mwezi Novemba, 2024

"Sambamba na hilo, Serikali imeingia mkataba wa kuboresha rada za hali ya hewa zilizofungwa katika mikoa ya Dar es Salaam na Mwanza ili kuendana na teknolojia ya kisasa ya rada za hali ya hewa," amesema Prof. Mbarawa.

Ameongeza kuwa, Serikali kupitia TMA imefanikiwa kukamilisha ufungaji wa mitambo mitano ya kutoa huduma za hali ya hewa katika viwanja vya ndege vya Songwe, Zanzibar, Arusha na Songea, ili kuboresha huduma hizo kwenye usafiri wa anga.

"Taratibu za ufungaji mitambo mitatu ya kupima hali ya hewa kwenye viwanja vya ndege vya Musoma, Iringa na Mpanda, zinaendelea", amesema Mbarawa.

Pia, Serikali imekamilisha ununuzi wa seti 28 za mitambo ya kupima hali ya hewa inayojiendesha yenyewe ambayo imefungwa katika vituo vya hali ya hewa vilivyopo kwenye viwanja vya ndege vya Mtwara, Songea na Arusha, huku mitamboi mingine 25 inaendelea na maandalizi ya kufungwa katika mikoa mbalimbali ikiwemo Morogoro, Iringa, Njombe, Tanga, Dodoma, Singida na Kilimanjaro.

“Kuhusu kuboresha mazingira ya kufanyia kazi na kujenga uwezo kwa watumishi, Serikali kupitia TMA imeendelea na ujenzi wa jengo la ofisi ya Kanda ya Mashariki na Kituo cha Tahadhari ya Matukio ya Tsunami, ambapo utekelezaji wake umefikia asilimia 39. Vilevile, watumishi 74 wanaendelea na mafunzo ndani na nje ya nchi katika ngazi mbalimbali za elimu,” amesema Prof. Mbarawa.

Aidha Prof. Mbarawa amesema TMA inaendelea kufanya tafiti mbalimbali za masuala ya hali ya hewa na mabadiliko yake na tabia ya nchi, ambapo tafiti nne zilichapishwa katika majarida ya kimataifa ya kisayansi.

Miongoni mwa tafiti hizo ni kuhusu tathimini ya matukio ya hali mbaya ya hewa katika Bahari ya Hindi, tathimini ya ongezeko la joto kwa kipindi kati ya 1982 hadi 2022, tathimini ya hali ya mvua katika vituo vya hali ya hewa nchini na tathimini ya mabadiliko ya mvua na athari zake katika kilimo kwa nchi za Afrika Mashariki.

Pia, Prof. Mbarawa amesema kutokana na umahiri wa mamlaka hiyo kwenye utoaji wa huduma za hali ya hewa, 2019 WMO iliichagua Tanzania kupitia TMA kuendesha kituo cha kanda cha kutoa mwongozo wa utabiri wa hali mbaya ya hewa kwa nchi zilizopo ukanda wa Ziwa Victoria.

“Kituo hicho kipo Dar es Salaam na kinahudumia nchi tano ambazo ni Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, na Burundi. Sambamba na hilo, TMA iliteuliwa kutekeleza jukumu la kufuatilia ubora wa takwimu za hali ya hewa (data) zinazopimwa katika vituo vya hali ya hewa vya nchi sita (6) vya ukanda wa Afrika Mashariki ikujumuisha nchi ya Sudan Kusini,” amesema Prof. Mbarawa.

Prof. Mbarawa ameongeza kuwa, katika kuhakikisha kuwa umma wa Watanzania unapata taarifa sahihi za hali ya hewa, TMA imeongeza wigo wa kuhabarisha umma kwa kusaini mikataba ya utangazaji wa taarifa za hali ya hewa na Redio tano (5) za jamii ambazo ni Jambo FM (Shinyanga), Harvest FM (Pwani), Inland FM (Mwanza), Revival FM (Manyara) na CGFM (Tabora) na kuwa na jumla ya vyombo vya habari 108 vinavyohusisha redio 80, Televisheni 17, magazeti matatu (3) na Televisheni Mtandao (on-line TV) nane (8).

 

 


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka Wakuu wa Mikoa nchini waakisi utashi wa kisiasa wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kusimamia na kutekeleza mapendekezo yote yaliyotolewa na Tume ya Haki Jinai.
 
“’Utashi wa kisiasa wa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuboresha mfumo wa utoaji wa Haki Jinai lazima udhihirike kwenu ninyi viongozi mlio karibu na wananchi. Hata hivyo, utashi huo hauwezi kudhihirika kwenu iwapo hamtakuwa na nia ya dhati ya kubadilika na kisha kuongoza mabadiliko kwenye maeneo mnayomwakilisha Mheshimiwa Rais wetu na hususan katika kuhudumia wananchi,” amesema.
 
Ametoa wito huo leo (Jumatatu, Mei 6, 2024) wakati akifungua warsha ya Wakuu wa Mikoa na Makatibu Tawala wa Mikoa ya kuwajengea uelewa kuhusu maboresho kwenye mfumo wa Haki Jinai na utoaji wa haki nchini kwenye ukumbi wa mikutano wa Tume Huru ya Uchaguzi, uliopo Njedengwa, nje kidogo ya Jiji la Dodoma.
 
Amesema sambamba na suala la utashi, ni lazima viongozi na watendaji wa Serikali wawe na uelewa wa kutosha ili waweze kuyasimamia na kuyatekeleza mapendekezo hayo.
 
Amesema malalamiko ya wananchi katika masuala kadhaa ndiyo yaliyoweka msukumo kwa Mheshimiwa Rais kuunda Tume ya Haki Jinai na kuyakubali mapendekezo yaliyotolewa na Tume hiyo na hatimaye kuigeuza kuwa Kamati ya kuandaa mikakati utekelezaji wa mapendekezo ya Tume ya Haki Jinai.
 
“Hivyo basi, kwa kuwa ninyi ni wawakilishi wa Mheshimiwa Rais katika maeneo yenu ya utawala, ni wajibu wenu kuhakikisha kuwa azma ya Mheshimiwa Rais inatimia kwa kusimamia na kutekeleza mapendekezo yote yaliyotolewa na Tume ya Haki Jinai,” amesisitiza.
 
Akitaja masuala yaliyolalamikiwa na wananchi, Waziri Mkuu amesema utungaji wa baadhi ya sheria ndogo katika mamlaka zao ambazo aghalabu hukinzana na sheria mama. “Mfano ni tozo zinazoanzishwa na halmashauri kama vile ushuru wa mabango, kodi za maegesho na usimamizi wa matumizi ya maeneo ya barabara zinasababisha mkanganyiko kwa wananchi kwa kuwajibishwa na chombo zaidi ya kimoja,” amesema.
 
Masuala mengine ni migogoro ya ardhi, matumizi mabaya ya madaraka ya ukamataji na desturi kwa Wakuu wa Mikoa na Wilaya kuambatana na Wajumbe wa Kamati za Ulinzi na Usalama katika ziara mbalimbali hata zile zisizohitaji uwepo wa vyombo hivyo, hali ambayo imekuwa ikisababisha hofu kwa wananchi na kuwafanya washindwe kufikisha mawazo na kero zao kwa viongozi hao.
 
Amewataka viongozi wote walioshiriki warsha hiyo wazingatie maelezo yatakayotolewa ili kila mmoja akawe chachu ya mabadiliko ya kifikra, kimtizamo na kiutendaji katika eneo lake. “Wakuu wa Mikoa na viongozi wote mlioshiriki katika warsha hii, endeleeni kushirikiana na taasisi za Haki Jinai katika utekelezaji wa mapendekezo ya Tume ya Haki Jinai ya kuboresha mfumo na utendaji wa taasisi hizi.”
 
Amewataka wazingatie uwepo wa majengo na miundombinu muhimu kwa ajili ya taasisi za Haki Jinai katika maeneo mapya ya utawala (Wilaya) yaliyoanzishwa. “Kuna maeneo mengi mapya ya utawala bado huduma za Haki Jinai kama vile vituo vya Polisi na magereza hazijafika na wananchi wanapata taabu sana kuzifikia huduma hizo katika Wilaya mama ikiwemo kutembea au kusafiri kwa muda mrefu,” amesisitiza.
 
Mapema, Naibu Waziri Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Dkt. Festo Dugange alisema kuwa ofisi hiyo itasimamia utekelezaji wa maagizo na maelekezo yatakayotolewa katika warsha hiyo ili dhamira ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuona wananchi wanapata haki zao inafikiwa.
 
“Naomba nitumie nafasi hii kukuhakikishia kuwa yote ambayo tutajifunza katika warsha hii na maelekezo yote ambayo Mheshimiwa Waziri Mkuu utatupa tutahakikisha tunakwenda kuyatekeleza katika mikoa na halmashauri zetu ili dhamira ya mapendekezo ya Tume ya Haki Jinai yaweze kufikiwa.”   
 
Naye, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Jaji Mkuu Mstaafu Mohamed Othman Chande alisema Kamati yao iliundwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Septemba 2023 ili kufanyia kazi ripoti ya Tume iliyokuwa na mapendekezo 333 ya maboresho ya utendaji kazi wa taasisi za haki jinai katika maeneo mbalimbali.
 
Alisema takwimu zinaonesha kuwa matukio ya uhalifu nchini yanazidi kuongeza mwaka hadi mwaka na kwamba juhudi kubwa zinaelekezwa kupambana na uhalifu badala ya kubaini na kuuzuia.
 
“Moja ya majukumu tuliyopewa kwenye kamati hii ni kuandaa Mkakati wa Kitaifa wa Kubaini na Kuzuia Uhalifu unaotarajiwa kuwa nyenzo ya utekelezaji wa taasisi na mamlaka zote zinazohusika ili kukabiliana na janga la uhalifu nchini,” alisema na kuongeza kuwa viongozi na watendaji wote watakuwa na jukumu la kusimamia utekelezaji wa mkakati huo utakaporidhiwa na Serikali ili malengo yake yaweze kutimia.
 
Mada zinazowasilishwa kwenye warsha hiyo ni: Kujenga Uelewa wa Mapendekezo ya Tume ya Haki Jinai; Mfumo wa usimamizi, Kujenga Uelewa wa namna ya kutekeleza Mapendekezo ya Tume ya Haki Jinai; Mfumo wa usimamizi ufuatiliaji na uwajibikaji wa Viongozi na Watendaji na kuzingatia weledi, maadili na rushwa katika kuhakikisha upatikanaji wa haki.




 

 

Na Mwamvua Mwinyi, Rufiji

MKUU wa wilaya ya Rufiji, Meja Edward Gowelle ametoa agizo kwa watu ambao bado wanaoishi kwenye maeneo yaliyozingirwa na maji ,mabondeni waondoke na kuhamia kwenye maeneo yaliyotengwa na Serikali kwa ajili ya usalama wao.

Akipokea misaada mbalimbali yenye thamani ya milioni 28 kutoka Taasisi ya WHO IS HUSSAIN, kwa ajili ya waathirika wa mafuriko Rufiji, Gowelle alisema, Serikali inaendelea kutoa maeneo ya kutosha ili kuhakikisha wapo salama.

Alieleza ,kijiji cha Chumbi kimetoa eneo, kwasasa wanaendelea kulipima litakuwa na viwanja 500 kwa ajili ya makazi yaliyo salama.

Aidha Gowelle alieleza, wakala wa huduma za misitu Tanzania (TFS) imetoa eneo Muhoro, na Serikali kutoa kwa wananchi ambapo vimetengwa viwanja 600 .

Alieleza, kazi kubwa inaendelea kufanyika kwani mvua bado zinaendelea kunyesha.

Vilevile alifafanua kwamba, katika kambi ya Chumbi kulikuwa na waathirika wa mafuriko 498 sasa wamebakia 311 ,kaya zilikuwa 117 kwasasa zimebakia 82.

"Watu wote 89,000 wengine wapo kwa ndugu, jamaa na marafiki,nao hao tunaendelea kuwawezesha kwasababu kwa hali ya kawaida kama mtu ukipokea kaya 3 zenye watu 11 alikuwa anakula debe mbili, hivyo kwasasa atahitaji debe 10 ,kwahiyo misaada hii tunayopokea tunashukuru Sana wadau hawa" alisema Gowelle.

Alisema, mafanikio hayo yametokana na mh Rais Samia Suluhu Hassan ameonyesha uwezo wake mkubwa katika kujenga mahusiano na Taasisi ndani na nje .

Gowelle alimpongeza Rais Samia kwa kutoa tani 300 za chakula, kupeleka vifaa tiba,madawa kupitia MSD kudhibiti magonjwa ya mlipuko.

Alimshukuru Mbunge wa Jimbo la Rufiji, Mohammed Mchengerwa kwa jitihada zake za kutafuta wadau,ambapo hadi sasa imefikia milioni 107.7 fedha ambayo wataenda kununulia mbegu ,mchakato umeanza ili baadae waathirika wanaojishughulisha na kilimo warejee kwenye kilimo na yeye amechangia milioni 50.

Akizungumza baada ya kukabidhi misaada kambi ya Chumbi, mratibu wa mradi wa Taasisi ya WHO IS HUSSAIN ,Mohsin Bharwani alisema ,WHO IS HUSSAIN inajishughulisha na kusaidia jamii katika mambo mbalimbali ikiwemo kujenga visima, shule.

"Wakati changamoto ya mafuriko inaanza tulimuona kwenye vyombo vya habari Mbunge wa jimbo Mchengerwa akitoa misaada na kuomba wadau kushirikiana na Serikali kuchangia waathirika "alisema Mohsin.

Mohsin alisema, wameguswa na kuanza kuchangishana na washirika wao wengine na kufanikiwa kupata misaada hiyo.

Kwa upande wake Fatema Kermali kutoka WHO IS HUSSAIN alisema,wametoa mchele kilo 2,000, magodoro 110, maharage 900,sukari 1,400 ,sembe 1,500,mafuta lita 1,200,pedi, miswaki na sabuni vyote vina thamani ya Mil.28.

Kwa mujibu wa tathmini ,Wilaya ya Rufiji ni moja ya wilaya nchini iliyokumbwa na changamoto ya mafuriko kwa kiasi kikubwa,na kuathiri kata 12 kati ya 13 zilizopo, kusababisha vifo 8 , waathirika 89,000, kaya 23,360,makazi,Nyumba 628.



 


Na Mwandishi Wetu

Serikali imetenga kiasi cha TZS bilioni 18.5 kwa ajili ya kuwawezesha wajasiriamali nchini zitakazotolewa kama mikopo yenye masharti nafuu kupitia Benki ya NMB.

Makubaliano ya utaratibu wa ufadhili huo yalitiwa saini leo jijini Dar es Salaam na Afisa Mtendaji Mkuu wa benki hiyo, Bi Ruth Zaipuna, na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Seif Abdallah Shekalaghe kwa niaba ya Serikali na kushuhudiwa na mkuu wa wizara hiyo, Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima.

Akizungumza kabla ya utiaji saini ya mkataba huo wa miaka miwili, waziri huyo alisema wafanyabiashara wadogo na wa kati watakopeshwa fedha hizo kwa riba ya asilimia saba.

“TZS bilioni 18.5 ni hela nyingi za kuanzia lakini kiasi hiki kitaongezeka kwani lengo la Serikali ni kuifanya mikopo hii kuwa endelevu ili iwafikide watu wengi,” Dkt Gwajima alibainisha huku akisisitiza umuhimu wa kuitumia vizuri na kuirejesha kwa wakati.

Aliongeza kuwa fedha hizo zikiwekezwa vizuri zinaweza kuwa na tija kubwa kimaendeleo kwa kusaidia kuchochea ukuaji wa uchumi na kuboresha mapato ya kaya.

Dr Gwajima alisema mikopo hiyo ni sehemu ya utaratibu mpya wa Serikali kuyawezesha makundi maalum na kuhakikisha wanufaika wake ni wale tu waliolengwa kupata usaidizi huo.

“Wajasiriamali na wafanyabiashara wadogo wana mchango mkubwa katika maendeleo ya nchi kwa hiyo Serkali kupitia wizara hii ina kila sababu ya kuwakwamua na kuwawezesha ikiwemo kupitia mikopo hii nafuu ambayo NMB imeanza kuitoa leo.”

Kwa mujibu wa Dkt Shekalaghe utiaji saini na NMB kukopesha fedha hizo kumeitimisha mchakato wa wizara yao kuitafuta benki mshirika katika masuala mbalimbali ya kiutendaji na kimaendeleo.

Akibainisha kuwa mafungu ya mikopo hiyo nafuu itatoka kila mwaka, katibu mkuu huyo alisema Serikali imeanzisha utaratibu mpya wa kuyafadhili makundi maalumu na tayari uandikishaji ya wale wenye sifa stahiki umeanza na kwa upande wa wajasiriamali pia wanapewa vitambulisho maalum.

Katika maelezo yake, Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB, Bi Ruth Zaipuna alisema mkataba wa kutoa mikopo hiyo ni kielelezo cha jitihada kubwa zinazofanywa na benki hiyo kuunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita kuboresha mazingira ya biashara kwa wafanyabiashara wote nchini wakiwemo wale wadogo.

Aidha, alisema benki hiyo ina uzoefu na uwezo mkubwa wa kuwahudumia wajasiriamali ambao umeifanya kutambulika kimataifa kama kinara wa kuzifadhili biashara changa, ndogo na za kati nchini.

“Tuzo tulizozipata mwaka huu katika hilo ni pamoja na zile za Benki Bora ya Wafanyabiashara Wadogo na wa Kati na Benki Bora ya Uwezeshaji wa Biashara Ndogo na za Kati,” Bi Zaipuna alisema.

“Ukweli huo unadhihirishwa na idadi ya mikopo 129,540 yenye thamani ya TZS trilioni 2.03 iliyotolewa na NMB kwa wajasiriamali kwa kipindi cha mwaka 2020 hadi 2023,” aliongeza na kueleza kuwa ukopeshaji huo kwa wajasiriamali wakiwemo wamachinga na boda boda ulikuwa ni wastani wa mikopo 2,699 kila mwezi na TZS bilioni 42.3 kwa mwezi.

“Historia ya Benki ya NMB imejengwa kupitia uwezeshaji wa sekta ya biashara ndogo na za kati, kutoa mikopo na juhudi za kuwafikia wafanyabiashara ni moja ya vipaumbele katika mpango mkakati wetu,” alifafanua.

Bi Zaipuna alimwambia Dkt Gwajima kuwa utiaji saini mkataba kati ya NMB na wizara yake kutapanua wigo wa kuwafikia wafanyabiashara wengi zaidi wanaojishughulisha na biashara ndogo ndogo nchini.

Pia alisema taasisi hiyo inajivunia kushirikishwa na Serikali kupitia Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum katika utekelezaji wa mipango ya kuwahudumia wajasiriamali kwa lengo la kukuza biashara zao na kuwapa fursa ya kuchangia ukuaji wa uchumi wa nchi na pato la taifa kwa ujumla.

Akisisitiza umuhimu wa wajasiriamali katika maendeleo, Bi Zaipuna alisema shughuli zao ni zaidi ya asilimia 95 ya biashara zote rasmi duniani zikichangia asilimia 50 ya pato la taifa kwa nchi za Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara na zaidi ya asilimia 80 ya ajira zote barani Afrika.

“Pamoja na utoaji mikopo tunaamini kuwa wafanyabiashara hawa watafaidika pia na huduma nyingine mbalimbali za kifedha zinazotolewa na benki yetu na hivyo kuwafanya wakue kibiashara,” alibainisha huku akitilia mkazo umuhimu wa kuwapa elimu ya fedha ili kuhakikisha wanakuwa na nidhamu nzuri ya matumizi ya mikopo hiyo.












Wanafunzi kutoka Chuo Kikuu cha Antwerp Ubelgiji na Chuo Kikuu cha Kikristu cha Uganda ambao wapo katika programu ya kubadilishana Wanafunzi na Chuo kikuu Mzumbe wamewasilisha matokeo ya awali ya tafiti walizofanya kwenye maeneo ya maji, elimu na usalama wa chakula kwa kusimamiwa na wahadhiri wa Chuo Kikuu Mzumbe ikiwa ni sehemu ya mafunzo yao katika Shahada ya Umahiri ya Menejimenti ya ufuatiliaji na Tathmini.

Akizungumza katika semina ya uwasilishaji wa matokeo ya tafiti hizo iliyofanyika Chuo Kikuu Mzumbe Kampasi

Kuu Morogoro mwishoni mwa wiki, Mratibu wa Mradi wa ‘ICP connect’ unaotekelezwa kwa ushirikiano baina ya Chuo kikuu Mzumbe na Chuo Kikuu cha Antwerp, Ubelgiji Dkt. Christina Shitima amesema kuwa uwasilishaji wa matokeo ya tafiti hizo ni matunda ya mkataba wa ushirikiano kati ya Chuo Kikuu Mzumbe na Chuo Kikuu cha Antwerp vilivyokubaliana kushirikiana na kubadilishana wanafunzi na wanataaluma, kutengeneza programu pamoja na kufanya tafiti

Dkt. Shitima amesema kuwa uwasilishaji wa matokeo hayo ya awali umelenga kuisaidia Serikali na Wadau kuchukua hatua madhubuti ikiwemo kutunga sera na kufanya maamuzi ya kuboresha huduma za kijamii zikiwemo maji, elimu na usalama wa chakula ambazo tafiti zake ndio zinatolewa mrejesho na wanafunzi hao.

Katika hatua nyingine, wadau mbalimbali walioshiriki katika Semina hiyo ya kutoa matokeo ya awali wameeleza kuwa tafiti hizo zitaisaidia Serikali kuandaa vyema malengo, mipango na bajeti kwa ajili ya kuzitatua changamoto zilizoibuliwa na watafiti hao na hatimaye kuboresha huduma za kijamii kwa wananchi

“Tafiti hizi zina tija kubwa sana ikiwa zitawasilishwa kwa Serikali na mamlaka zenye dhamana kwani zitasaidia kuweka mipango bora ya kuzikabili changamoto zilizoibuliwa katika sekta ya maji, elimu na chakula. Hata hivyo, tayari Serikali imeshaanza kuchukua hatua katika bajeti inayokuja kwa kuweka mipango ya kuboresha miundombinu ya shule ya msingi ya Mongwe ambako ilikuwa ni moja ya sampuli za utafiti kwenye sekta ya elimu”. Alisema Diwani wa Kata ya Mlali Mhe. Frank Mwananzeche.

Naye Mhandisi wa Mamlaka ya Maji Wilaya ya Mvomero Mhandisi Mlenge Luperitilo amesema tafiti kama hizo zinawasaidia wao kama watendaji wa Serikali kubaini changamoto kwenye maeneo ambayo yana shida zaidi na pengine wameshindwa kuyafikia kwa wakati huo na hivyo kuwekeza nguvu zaidi katika kutatua changamoto za maji.

Mhandisi Mlenge amekishukuru Chuo Kikuu Mzumbe kwa kuwazesha wanafunzi hao kufanya tafiti hizo na amewaomba watafiti wengi zaidi kujitokeza ili kushirikiana na Serikali kutatua changamoto mbalimbali za wananchi hasa kwenye sekta ya maji.

Kwa upande wao Wanafunzi hao wa kimataifa wamesema wamefurahi kupata fursa ya mafunzo ya kufanya tafiti nchini Tanzania kupitia Chuo Kikuu Mzumbe ambacho wamekielezea kuwa ni chuo bora sana kwa masomo kwani kina mazingira mazuri na tulivu ya kujifunzia na kwamba wanaamini matokeo ya tafiti waliyoyawasilisha yataisaidia Serikali na Wadau kuboresha huduma, na hivyo watakuwa wametoa mchango wao wa kimaendeleo.

“Tumekaa hapa Chuo Kikuu Mzumbe kwa wiki tano za mafunzo, tumekuwa na wakati mzuri sana katika mafunzo ya darasani, tumepata fursa ya kubadilishana uzoefu na wanafunzi wenzetu, tumetembelea vijiji na kuzungumza na wanajamii tumepewa ukarimu wa hali ya juu na wenyeji wetu kuanzia waratibu, walimu na wanafunzi.Tumefurahi sana kujifunza Chuo Kikuu Mzumbe”. Alisema Fiona Ward Shaw, raia wa Marekani na Mwanafunzi wa Shahada ya Umahiri katika Menejimenti ya Tathmini na Ufuatiliaji anayesoma Chuo Kikuucha Antwerp kilichopo nchini Ubelgiji.

Naye Vicent Manimani raia wa Congo DRC na Mwanafunzi kutoka Chuo Kikuu cha Kikristu cha Uganda amesema wamepata uzoefu wa kutosha utakaowasaidia katika taaluma yao na amewakaribisha wanafunzi wengine kutafuta fursa ya kutembelea na kujifunza katika Chuo kikuu Mzumbe kwa kuwa ni chuo kizuri sana.

“Mzumbe ni njema sana kwa kujifunzia, ninawakaribisha watu wengine kutembelea na kujifunza hapa, hakuna matata”. Alisema Vicent Manimani.
Mkuu wa Mkoa wa Songwe Mhe. Daniel Chongolo ameipongeza timu ya wataalamu wa Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) kwa kufanya kazi kwa haraka na ufanisi mkubwa kuhakikisha barabara zinapitika mkoani Songwe.

RC Chongolo ameeleza kuwa changamoto ya uharibifu mkubwa wa miundombinu umefanyiwa kazi kwa haraka na timu ya wataalamu wa TANROADS na TARURA jambo ambalo limerejesha mawasiliano ya pande zote zilizokuwa hazipitiki.

"Kila mmoja kwa barabara zake wamefanya kazi kubwa na wanaendelea kufanya hivyo lengo ni kuhakikisha Wananchi hawakosi huduma ya barabara pale inapotokea changamoto’’ Amekaririwa Mhe Chongolo.

Kwa upande wake Meneja wa Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Songwe Mhandisi Suleiman Bishanga akizungumza mara baada ya kukagua sehemu zilizoathirika na mvua za El-Nino wilayani Songwe na Ileje amesema kuwa Serikali inayoongozwa na Rais Mhe Dkt. Samia Suluhu Hassan imetoa zaidi ya shilingi Bilioni 5.7 kwa ajili ya kutatua changamoto na kurejesha miundombinu ya barabara na madaraja ambayo yameharibiwa na mvua kubwa za El- nino zinazoendelea kunyesha Mkoani Songwe.

Amesema kuwa Wilayani Songwe miundombinu imeharibika katika barabara ya Galula – Namkukwe sehemu ya Malangali, daraja la Mpona maji yalifurika juu na kukata mawasiliano kati Kijiji cha Namkukwe na Mpona.

Sehemu nyingine ni Magamba eneo linalounganisha Kijiji cha Mpona na Igalula ambako sasa hivi linajengwa daraja na kuinua tuta la barabara; pia kwenye barabara ya Chang’ombe - Mkwajuni eneo la Zira miaka ya nyuma lilikuwa korofi; lakini mwaka huu halijapata changamoto kwa sababu Serikali kupitia TANROADS ilichukua hatua za mapema kulifanyia matengenezo.

Ameeleza kuwa Wilayani Mbozi Barabara iliyoathirika zaidi ni Mlowo – Kamsamba ambayo inaunganisha Mji wa Songwe kuelekea upande wa Mkoa wa Rukwa ambapo Serikali imetoa zaidi ya shilingi bilioni moja kutengeneza maeneo mbalimbali yaliyoharibika.

“Katika Wilaya ya Momba kuna barabara ambayo tumeirithi mwaka jana kutoka TARURA kuja TANROADS na yenyewe ilikuwa katika hali mbaya, Serikali haikusita ikatupa fedha shilingi milioni 500 ambazo zimeenda kushughulikia matatizo ya kule na sasa ile Barabara ya Kwenda Ilonga inapitika’’ ameeleza Mhandisi Bishanga na kuogeza.

“Wilaya ya Mbozi kuelekea Ileje kuna sehemu tunaunganishwa na Daraja la Hezya lile dadaja lilisombwa na maji na Serikali imetoa zaidi ya shilingi milioni 261 kwa ajili ya kujenga daraja hilo na kwa sasa linapitika’’.

Kwa upande wao Afisa Tarafa ya Songwe Godwin Kaunda na Diwani kata ya Magamba Mhe Kapala Chakupewa Makelele wameishukuru serikali kupitia TANROADS kwa urejeshaji wa haraka kwa miundombinu ya barabara na madaraja iliyoathiriwa na mvua za El-Nino zinaendelea kunyesha katika maeneo mengi nchini.









Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama (Mb) Peramiho akizungumza katika sherehe za jumuiya ya Wazazi zilizofanyika kiwilaya katika Kijiji cha Kilagano Halmashauri ya wilaya Songea.Na Maandishi wetu
WAZIRI  wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama (Mb) Peramiho amewataka wazazi kutenga muda malezi kwa watoto ili kuwatizama na Kurekebisha mienendo yao.

Kauli hiyo ameitoa mapema Leo tarehe 05/05/2024 Wakati aliposhiriki kama Mgeni rasmi maadhimisho ya miaka 69 ya Jumuiya ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi wilaya ya Songea Vijijini, sherehe zilizofanyika katika Kijiji cha Kilagano katika Halmashauri ya wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma.

Waziri amesema, mtoto anayelelewa kwa kuangalia mfano mzuri wa baba na mama lazima atakuwa na nidhamu na tabia njema.

"Wazazi tukae tutafakari utaratibu tunaotumia kulea watoto wetu ili wawe na madili bora katika katika Jamii,"alibanisha.

Ameeleza kwamba lengo la kuanzishwa Jumuiya ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi ni kuhakikisha inajenga maadili mema ndani ya chama na taifa kwa ujumla.

Niendelee kuhimiza Viongozi wa jumuiya ya wazazi ndani ya wilaya kwenye Kata na kwenye matawi na kwenye Mashina tuendelee kulibeba jukumu hili.

"Kizazi kilichopo na hata kizazi kipya kimeathirika na maswala ya utandawazi, na nguvu mpya ya Mawasiliano kama isipotumika vizuri itakuwa ni chanzo cha upotofu wa maadili," alisema Waziri Mhagama.

Tunahitaji wanachama wenye maadili, tunahitaji wananchi wa Peramiho wenye maadili, alifafanua.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Songea Vijijini Mhe. Menace Komba ameishukuru Serikali na juhudi za Mhe. Mbunge Mhe. Jenista Mhagama, walizofanya za kurekebisha Mpaka wa Mlima Lihanje.

Tulifanya Mkutano na timu ya Mawaziri na tulifanya Mkutano Kilagano na kuzungumza na wananchi na baadae kufanikiwa kurekebisha mipaka ya Mlima Lihanje.

"Serikali ya wilaya itahakikisha wananchi walioathirika na zoezi hilo kwa kuondolewa kwenye Mlima na kuwarudisha chini wanapata ardhi iliyotengwa kwa usawa," alisema.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama (Mb) Peramiho akifurahia Jambo na Viongozi wa Jumuiya ya Wazazi katika sherehe yao iliyofanyika kiwilaya katika Kijiji cha Kilagano Halmashauri ya wilaya ya Songea.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge na Uratibu ) Mhe. Jenista Mhagama (Mb) Peramiho akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa jumuiya ya Wazazi mara baada ya kuhitimisha sherehe yao iliyofanyika katika Kijiji cha Kilagano Halmashauri ya wilaya ya Songea.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama (Mb) Peramiho akifurahia Jambo na wakinamama walioshiriki kutumbuiza sherehe za Jumuiya ya Wazazi za Chama Cha Mapinduzi zilizofanyika kiwilaya Katika Kijiji cha Kiagano Halmashauri ya wilaya ya Songea.

Top News